Monday, November 10, 2014

Miss Tanzania Mpya 2014 Lilian Kamazima Yadaiwa Ni Mnyarwanda, Apondwa Kuwa Ni Mbaya.

Lilian Kamazima
Mwenzako akinyolewa wewe tia maji !......Zengwe jipya limeibuliwa jana na kuenezwa kwenye mitandao ya kijamii kwamba Lilian Kamazima aliyepewa taji hilo baada ya Sitti Mtemvu ambaye ni mshindi wa awali kujivua taji kutokana tuhuma za kudanganya umri, si raia wa Tanzania bali ni Mnyarwanda.
Hashim Lundenga ambaye ni Mkurugenzu wa Miss Tanzania, amekanusha vilivyo na kusisitiza kuwa ni uzushi kwa sababu wao wanaangalia vyeti vya kuzaliwa ambavyo vinaonyesha uraia wa mshiriki.
Hayo yameibuka siku mbili tangu Lilian kukabidhiwa taji la Miss Tanzania 2014, lililokuwa likishikiliwa na Sitti Mtemvu aliyeamua kulivua baada ya kukumbwa na kashfa mbalimbali tangu kutawazwa kwake Oktoba 11.
Ukiachilia mbali hilo la uraia tangu apewe taji hilo juzi kwenye mitandao ya kijamii mashabiki wa urembo wamekuwa wakimponda Lilian kuwa ni mbaya sio mzuri wa kuwa Miss Tanzania.
Lilian ambaye awali alikamata nafasi ya pili kwa mujibu wa Mwanaspoti alisema: “Sikuwa na kinyongo ukizingatia urembo ni mambo mengi si sura, ngozi, mwonekano pekee bali unajumuisha mambo mengi, ndiyo maana kipindi cha usahili huwa kirefu. Binafsi niliamini kwamba (Sitti) alistahili hasa kutokana na kuwa na vigezo vingi vinavyoonekana kwa macho hata tulipokuwa kambini, nilikubali matokeo,”
Lilian alisema kipindi cha mwezi mmoja tangu kutolewa kwa matokeo Oktoba 11, anaamini kilikuwa kigumu kwa Sitti, pia kwake hasa ukizingatia tuhuma mbalimbali zilizokuwa zikimkabili mrembo huyo aliyetokea katika Kanda ya Temeke.
“Nina maono ya mbali na ninatamani miaka mitano ijayo niione Tanzania iliyokua hasa katika nyanja ya elimu, napenda kuona namba ya wanafunzi wanaofaulu ikiwa sawa vijijini na mijini ili kuwa na taifa lenye watu werevu na wenye maendeleo, hivyo nitajitahidi kutumia nafasi yangu kusongesha gurudumu hili,” alisema.
Mrembo huyo ambaye kwa sasa yupo nchini Uganda kwa shughuli za masuala ya mitindo, alisema anafurahia kupata nafasi hiyo na anawaahidi Watanzania kuwa atafanya kazi kwa nguvu zote ili kuhakikisha anatimiza malengo ya waandaaji wa mashindano hayo. Lilian Kamazima ana miaka 18, alishiriki akitokea Mkoa wa Arusha.

No comments:

Post a Comment